Friday, 12 June 2015

KARIBUNI WOLVERHAMTOM CAFE










WATANZANIA WATIKWA KUENDELEZA UTAMADUNI WAO

Na Aboud Mahmoud,Zanzibar
IPO haja kwa wananchi wa Tanzania kuendeleza na kudumisha utamaduni wao ili kuweza kujitangaza kitaifa na kimataifa pamoja na kuvuta watalii wengi ili kuja kuona tamaduni zao.
Hayo yamesemwa na Balozi wa Uswiss ambae amemaliza muda wake Olivier Chave, katika sherehe za kutimiza miaka 14 ya Chuo cha Muziki wa Nchi za Jahazi Zanzibar (DCMA)  pamoja na kumuaga yeye mwenyewe ambae ni mfadhili  mkuu wa chuo hicho.
Alisema kwamba utamaduni wa nchi ndio kitu muhimu ambacho watu wengi kutoka nchi mbali mbali hupenda kukijua na kuvutia watalii wengi ambao huongeza mapata ya nchi.
Alisema kwamba zipo nchi nyingi duniani zimekuwa zikipata wageni wengi kupitia kukuza utamaduni wao pamoja na kuutangaza ndani na nje ya nchi kutokana na kushirikiana baina ya wananchi na Serikali.
“Nawaomba wafanyabiasha, na wadau wa sekta mbali mbali kuunga mkono utamaduni wa Zanzibar kwani tukiiwachia Serikali na wasanii peke yake nchi hii haitoweza kujitangaza na kupata mafanikio ya aina mbali mbali,”alisema.
Aidha balozi Chave aliikisifia chuo cha DCMA kwa kuwa mstari wa mbele kuwarithisha vijana wa Kitanzania katika utamaduni wa mambo mbali mbali ikiwemo ngoma za asili.
Hivyo aliwashauri walimu na uongozi wa bodi hiyo kutochoka katika kuwarithisha vijana hao na sanaa ambayo inahitaji kuendelezwa katika kuitangaza Tanzania na Zanzibar kwa ujumla kitaifa na kimataifa.

Katika sherehe hizo mabzo zilifanyika katika chuo hicho kulifuatiwa na burudani  mbali mbali ikiwemo taarab, na ngoma za asili. 

BALOZI SEIF: DUMISHENI NIDHAMU KWENYE MICHEZO

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amehimiza umuhimu wa wanamichezo kuendelea kudumisha nidhamu michezoni ili kulijengea sifa
Bora Taifa katika sekta hiyo kwa kuwa na wanamichezo walishiba maadili na heshima iliyotukuka.

Balozi Seif Ali iddi alitoa himizo hilo wakati alipokuwa akizungumza na wachezaji pamoja na Viongozi wa Timu ya Soka ya Taifa ya Jang’ombe { Wakombozi wa Ng’ambno } katika hafla ya kukabidhiwa Kikombe cha ubingwa baada ya Timu hiyo kupanda Daraja la kwanza Kanda mwaka huu.
Alisema nidhamu na heshima ndio kitu pekee kilichosababisha wachezaji wa enzi zilizopita hapa Zanzibar kuwika na hatimae kuiletea sifa Zanzibar katika ulimwengu wa kabumbu.

Balozi Seif alieleza kwamba Vijana wa sasa wana nafasi pana ya kuendelea kujifunza mbinu mbali mbali za michezo na hatimae kuwa mastaa ambazo hupatikana kupitia kwenye vipindi vya Televisheni pamoja na mitandao.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza wachezji pamoja na Viongozi wa Timu ya Soka ya Taifa ya Jang’ombe kutokana na kazi kubwa waliyoifanya na hatimae kuchukuwa ubingwa kwa kuingia daraja la Kwanza Kanda.

Balozi Seif alisema juhudi za wachezaji hao kwa upande mwengine zimeanza hatua mpya ya kujijengea uwezo wa kupata ajira kupitia mchezo wa soka ambao unaonekana kupendwa sana Duniani.

“ Wapo wachezaji maarufu wanaochezea timu zinazotajika Duniani katika ulimwengu wa kabumbu ambapo wengine wanatokea hata mataifa ya Afrika yanayolingana kiwango cha soka na Tanzania “ Alisema Balozi Seif.

Katika kuunga mkono wanamichezo hao wa Timu ya Soka ya Taifa ya Jang’ombe Balozi Seif ameahidi kuisaidia Timu hiyo Seti mbili za Jezi pamoja na Mipira Minne na akawataka wajiwekee malengo zaidi ya kufanikiwa katika fani yao hiyo kwa siku zijazo.

“ Wale Jamaa wakikuoneni mnavyolisakata soka sawa sawa kikweli watafikia hatua ya kukununueni tuu na kwa upande mwengine Zanzibar tutakuwa na haki ya kujigamba kwamba tumetoa wachezaji wanaouwezo wa kuchezea timu za Kimataifa “. Alisema Balozi Seif.

Akizungumzia suala ya ujenzi wa Jengo la kudumu la Timu hiyo ya Taifa ya Jang’ombne Balozi Seif aliwashauri Viongozi na wachezaji hao kuanza ujenzi wa msingi na yeye atakuwa tayari kusaidia matofali kwa hatua ya kunyanyua.


Alisema uwezo wa kujenga jengo lao uko mikononi mwao ambapo viongozi wao jukumu lao kubwa ni kuhakikisha kwamba wanasaidia nguvu na maarifa ili kuona malengo waliyojipangia yanakwenda hatua baada ya hatua.

Mapema Rais wa Timu ya Soka ya Taifa ya Jang’ombe Salim Ridhiwani alisema Uongozi wa Klabu hiyo umeamuwa kuimarisha Timu hiyo ili kurejesha heshima na hadhi ya klabu hiyo iliyopotea katika miaka ya hivi karibuni.

Ridhiwani alisema Wanachama wa klabu hiyo wanajivunia maendeleo makubwa yaliyopatikana ndani ya klabu hiyo hasa kutokana na wachezaji wa timu hiyo kuiwezesha timu yao kuyakabili mashindano makubwa ya Kombe la Mapinduzi na kutoa upinzani mkubwa kwa timu zenye uzoefu wa mashindano ya soka Kimataifa.

Naye Mwakilishi wa Jimbo la Mpendae Mohammed Said Dimwa alisema Uongozi wa Jimbo hilo umeifufua tena Timu hiyo ndani ya Kipindi cha miaka Miwili iliyopita baada ya kufifia kutokana na changamoto kadhaa zilizokuwa zikiikabili timu hiyo katika miaka ya nyuma.

Dimwa aliahidi kwamba yeye pamoja na viongozi wenzake watasimama imara katika kuhakikisha Timu hiyo inarejea katika hadhi yake iliyopewa na wapenzi wa timu hiyo ya kuitwa wakombozi wa Ng’ambo.

Timu ya Taifa ya Jang’ombe { Wakombozi wa Ng’ambo } ilipanda Daraja na kushiriki mashindano ya Daraja la Kwanza Kanda mwaka huu baada ya kuifunga Timu ya Soka ya Maungani Goli 1-0 katika mchezo wa Mwisho wa mashindano ya Ligi Daraka la Pili.







RUKIA RAMADHANI: MSANII ASIEPENDA KUITWA MALKIA WA MIPASHO


“NIKUMBATIE mwenye wivu atazame,Nikumbatie roho yake imuume
Nikumbatie mwenye  wivu alalame,Nikumbatie akujue wangu mume
Njiani nikipita arudi kinyume nyume,Kata kiu yeye Fanta mi sina habari nae
Ajijue cheo chake mina yeye hatufanani,Atuone ashituke anijue mimi nani
Cheza na mimi mpenzi cheza name kwa helenzi,Mambo mazuri laazizi ndo hayataki haraka”
Ni moja ya beti katika nyimbo maarufu za muziki wa taarab visiwani Zanzibar na Tanzania kwa ujumla wa wimbo unaojulikana kwa jina la ‘Nikumbatie’ ambao uliimwa katika kundi maarufu la East African Melody.
Maneno hayo ni miongoni mwa wimbo mzima ulioghaniwa na mwanadada mwenye sauti ya kumtoa nyoka pangoni sie mwengine bali ni bibie Rukia Ramadhani Ali.
Rukia ni msanii mahiri katika anga la muziki wa taarab ndani nan je ya Tanzania ambae kila kona ya dunia anajulikana kutokana na kipaji chake alichojaaliwa na muumba wake.

Msanii huyo ambae hapendelei kuitwa malkia wa mipasho  kutokana na kutopendelea kuimbwa nyimbo za kupashana na kuelekeza zaidi nguvu zake katika nyimb o za mahaba na kubembeleza.
Nilipomuuliza anajiskiaje kuitwa jina hilo la malkia wa mipasho,hakuonesha bashasha wala haiba yake ya kawaida ya kutabasamu na akajibu ‘sitaki kuitwa malkia wa mipasho kwa sababu siimbi wala sifikirii kuimba mipasho’.
Jibu hilo lilinifanya nishangae kidogo kwa vile nyimbo za mipasho ndio zaidi hivi sasa zinazowapa umaarufu mkubwa  waimbaji wake kiasi cha kumuuliza nini sababu ya msimamo wake huo.
“Mimi ni msanii ninaependa zaidi taarab asilia ambayo lugha ya mashairi yake ni ya kiungwana,haina maneno makali tofauti na taarab ya kisasa,wanaimba tu lakini haina maadili ya Kizanzibari au taarab kwa ujumla,”alisema bila ya kutaka kuingia ndani zaidi.
Nilipotaka kujua alipoanzia hadi alipofikia,Rukia hakukataa tulikwenda hatua kwa hatua hadi mwisho wa mazungumzo yetu,alipoanzia alipofikia na matarajio yake ya baadae.
Msanii huyo alisema alijitosa rasmin katika fani ya muziki mwaka 1974 katikam kikundi cha Tawi la Afro Shirazi Party la Mwembeshauri chini ya mwalimu wake Marehemu Khamis Shehe.
Alisema wakati huo walikusanywa watoto wengi wa mtaani hapo kwa ajili ya kufundishwa masuala ya uimbaji na baada ya mafunzo ya muda walipelekwa majaji wenye uelewa mpana wa muziki huo na uimbaji kwa kuwachuja vijana hao.
Rukia alikuwa miongoni mwa vijanan waliopenya katika mchujo wa majaji hao na hapo ukawa mwanzo wa mafanikio  yake kwa vile kupita huko kulimfanya apelekwe katika klabu maarufu ya tab visiwani humu ya Culture Musical Club yenye maskani yake katika mtaa wa Vuga mjini Unguja.
Alianza mazoezi katika klabu hiyo na hatimae kuanza kuimba akiwa bado mwanafunzi wa shule na hivyo kuweza kubeba majukumu yake yote ya usanii na masomo shuleni.
Alisema alianza rasmin kuanza kupanda jukwaani akiwa na kundi lake la Culture na nyimbo yake ya kwanza ilijulikana kwa jina la ‘Kukupenda sana ndilo kosa langu sitofanya tena naapa kwa Mungu,Nilioyaona yanatosha kwangu’.
Kutoka kwake huko kuliwashtua wazazi wake ambao waliona kwamba anajikita zaidi katika maswala ya nuimbaji,badala ya kuzingatia masomo yake hivyo  ilimsababishia kuhamishwa Zanzibar na kupelekwa  Dar es Salaama kuendelea na masomo.
Msanii huyo mahiri alieleza kwamba alikaa jijini humo kwa muda wa miaka minne na kuendelea na masomo katika shule ya msingi ya Temeke kabla ya kurejea Unguja kuendelea na masomo yake katika shule ya Rahaleo,Kidutani ndogo na kubwa ambapo alimalizia kidato cha nne.

Kurejea kwake Unguja kulimfanya arudie tena kwenye muziki wa taarab na kwa bahati mbaya au nzuri hakurejea tena katika kundi lake la awali bali alihamia kwenye kundi mama la Nadi Ikhwan Safaa.
Alisema akiwa ndani ya kundi hilo,lenye maskani yake katika mtaa wa Kokoni mjini Unguja alikweza kuimba nyimbo kadhaa ambazo ziliweza kumjengea  jina na kumpa umaarufu zaidi.
Miongoni mwa nyimbo hizo ni pamoja na Nnazama, Nadra na Sadfa,Hidaya, Baada ya dhiki faraja,Niapishe na nyiengine nyingi ambazo zote hizo zinaendelea kupendwa hadi hivi sasa.
Rukia alisema kuanzishwa kwa kundi jipya la taarab la Bwawani ambalo lilikuwa linamilikiwa na hoteli ya Bwawani kulimfanya ahame katika kundi lake hilo na kuhamia katika kundi la Malindi chini ya msanii mahiri Marehemu Mwalimu Abdallah .
Alisema kikundi hicho cha Bwawani hakikudumu muda mrefu sana kwa vile kilivunjika,lakini kabla ya kuvunjika msanii huyo alifanikiwa kukiimbia kikundi hicho nyimbo kadhaa zikiwemo Nidhibiti,na Nadekea change.
Baadhi ya maneno yaliokuwemo katika nyimbo ya Nidhibiti ni kama hivi
Nidhibiti unitunze,Nitunze nihifadhike
Nihifadhi wanyamaze,Nipoe nitononoke
Raha zako nieneze,Milele milele nifarijike
Miti shamba wamalize,Halafu waweweseke.
Rukia ambae ni miongoni mwa wasanii waanzilishi wa kundi la ‘The East African Melody’ ambalo llilianzishwa nchini Dubae mwaka 1992,akiwa na wasanii kadhaa.
Akiwa nchini humo nyimbo za mwanzo alizoimba ni pamoja na Karibu habibi,Nimesharidhika na Nasubiri miujiza na baadae kundi hilo lilihama nchini Dubae na kuhamia visiwani Zanzibar.
Katikati ya mwaka 2000 msanii huyo alipumzika kuimba kwa muda wa mwaka mmoja hadi mwaka 2001 aliporejea tena kwenye ulingo wa taarab na kundi lake hilo la East African Melody.

Mara baada ya kurejea tena msanii huyo alionekana kuendelea kuvutia zaidi  kutokana na kuimba nyimbo zake kadhaa ambazo zilionekana kuvuta hisia za mashabiki wengi wa muziki wa taarab .
Miongoni mwa nyimbo hizo ni pamoja na Njoo Habibi,Nani kama wewe,Wastara hasumbuki,Kufa na tai shingoni,Nataka ridhaa yako,pamoja na nyimbo ya Nikumbatie.
Mbali na kuimba Rukia anamudu saana sanaa ya uigizaji ambapo aliwahi kuigiza mchezo wa ‘Mkombozi wa Mwafrika’ambapo alisema kwamba uimbaji uliweza kumletea matatizo kutoka kwa watu mbali mbali ikiwemo kumtishia kumpiga na hata wengine kutaka kumuwekea sumu kwenye chakula.
Pamoja na kutishiwa huko na vitisho hivyo msanii huyo alikabiliana na changamoto hizo ambazo hazikumkatisha tama na kuendelea na shughuli yake hiyo aliyokiri kuipenda ndani ya damu yake.
Rukia hakufafanua kwa nini alitishiwa,lakini alisema hayo ni mambo ya zamani na kwa sasa ayameshapita.
“Kwa kweli nilipokuwa najiunga na mambo ya sanaa nilipata tabu saana kwani nilitishiwa kupigwa na hata kuambiwa nitatiliwa sumu kwenye chakula lakini hayo yalikua mambo ya zamani sasa hivi hayapo,”alisisitiza.
Kuhusu maswala ya faida katika fani ya sanaa,Rukia alisema muziki wa taarab umeweza kumsaidia kupata faida nyingi ikiwemo umaarufu,kuheshimiwa na watu wa rika mbali mbali pamoja na kusafiri.

Alizitaja nchi alizotembelea kupitia muziki wa taarab ni pamoja na Mikoa mbali mbali ya Tanza nia,Kenya,Msumbiji,Comoro,Nigeria,Misri,Dubae,Oman,Abu Dhabi,Jamhuri ya Dominica,Ufaransa,Uswiss,Ubelgiji,Italia,Uholanzi,Slovenia,Ujerumani,Japan,Marekani na Uingereza.
Rukia alisema mpaka sasa kwa yeye ni taarab asilia ambayo ndio mwalimu wake katika fani hiyo lakini pia hiyo haimzuii kuimba taarab ya kisasa.
“Taarab asilia ndio taarab hizi nyengine tunaimba tu kufuata wakati,mimi siwezi kuidharau kwa kuwa ndiko nilipoanzia,”alifahamisha.
Akizungumzia juu ya tabia ya wasanii kuhama hama vikundi mara kwa mara ,alisematabia hiyo sio nzuri ,lakini ijulikane kwamba msanii hawezi kuhama bila ya sababu maalum.
Alijitolea mfano yeye mwenyewe kwamba kuhama kwake hakutokani na maslahi,bali kutokana na matatizo mbali mbali yaliokuwa yakijitokeza.
Msanii huyo hakusita kutoa shukurani zake za dhati kwa wasanii mbali mbali ambao walimuwezesha kudumu katika fani hiyo akiwemo marehemu Asha Simai,marehemu Khamis Shehe na Mohammed ilyas.
Kwa  vile hakuna msanii yoyote ambae hana msanii anaemvutia ,kwa upande wake Rukia alisema anavutiwa na uimbaji wa wasanii wengi akiwemo marehemu Asha Simai,Marehemu Abdulaziz Yussuf na Profesa mohammed Ilyas.
“Marehemu Bi Asha Simai alikuwa akinivutia mno katika fani yake ya uimbaji hasa nyimbo ya iwapi ile ahadi, inanisuuza roho yangu Namuomba Mwenyezi Mungu amsameh makosa yake,”alisema msanii huyo.
Hivi sasa Rukia Ramadhani ni muimbaji huru ambae anaimbia vikundi tofauti anapopata mualiko kikiwemo kikundi cha Zanzibar One Modern Taarab na vikundi vyengine.
Pia msanii huyo ni mwalimu wa sauti(kuimba) katika Chuo cha Muziki wa nchi za Jahazi(DCMA) ambapo aliwataka wasanii kujifunza zaidi  mara wanapoingia katika fani hiyo.
“Nawashauri wasanii kujifunza zaidi kusoma muziki ili waweze kujifahamu na kuelewa nini wanachokifanya jukwaani kwani wasanii wengi hawataki kujifunza.
Rukia Ramadhani Ali ni mtoto pekee wa bwana Ramadhani Ali na Bi Zuhura ambapo mbali na fani ya usanii lakini pia ni muajiriwa wa serikali katika Wizara ya Katiba na Sheria.


Thursday, 11 June 2015

WANAHABARI WATAKIWA KUTUMIA KALAMU ZAO ILI KUDUMISHA AMANI


WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kuacha kuandika habari ambazo zitakazosababisha kusababaisha vurugu na kuondosha amani iliyopo nchini Tanzania hasa  katika kipindi cha uchaguzi.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Zanzibar (ZAMEWO) Maryam Hamdani, wakati alipokua akifungua mafunzo ya siku mbili kwa wanahabari juu ya haki za binadamu na sharia za waandishi,huko katika ukumbi wa Kituo cha Huduma za Sheria.

Mwenyekiti huyo alisema kwamba nchi kadhaa duniani zimekuwa zikitokea kwa fujo kutokana na wanahabari kuandika habari ambazo zinahamasisha kwa wananchi kufanya vitendo ambavyo husababisha kuvunjiika kwa amani.

Alisema kwamba si vyema kuonekana nchi kama Tanzania ambayo ni nchi yenye amani kuharibika kutokana na maneno makali yanayozungumzwa na wanasiasa  na wanahabari kuyafikisha kwa jamii.

“Nakuombeni wanahabari wenzangu tuzitumie kalamu zetu kwa kuandika habari ambazo zitasaidia kudumisha amani iliyopo nchini kwetu na sio kuandika habari ambazo zitasababisha kuvunjika kwa amani,”alisema Mwenyekiti huyo.

Aidha aliseleza kuwa chuki za wanasiasa na maneno ya hasira yanayotoka katika midomo ya viongozi hao wa kisiasa yakiandiikwa katika na kutangazwa katika vyombo vya habari yanaweza kusababisha hali ya hatari katika nchi.

“Katika kipindi kama hichi cha uchaguzi hutokea mambo mbali mbali na kauli za kutisha na za hasira kutoka kwa wanasiasa,hivyo nakuombeni kuacha tabia ya kuandiika maneno hayo ili Tanzania isije ikawa kama Burundi au nchi nyengine,”alifahamisha.

Hivyo aliwataka wanahabari hao kusaidia kuwaelimisha wananchi kuleta na kuiendeleza amani iliyopo hapa nchini pamoja kuielimisha Serikali kulinda amani iliyopo.


Mafunzo hayo ya siku mbili kwa waandishi wa habari yameandaliwa na Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar (ZLSC) kwa kushirikiana na Chama cha Waa ndishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA).

ABDULWAKATI: NYOTA ISIYOSAHAULIKA KATIKA FANI YA SOKA NA TENISS


ZANZIBAR ni moja ya nchi ambazo zimejaaliwa kuwa na vipaji vya aina mbali mbali,vikiwemo vya utunzi,ufinyanzi na hata katika maswala ya michezo,ambayo kwa kiasi fulani ilitamba katika michezo ya aina tofauti.

Miongoni mwa watu waliotamba visiwani humu katika mchezo wa soka na mpira wa mezani Abdullah Juma Aley almaaruf Abdulwakati ambae aliweza kuitikisa Zanzibar nan chi nyengine duniani michezo hiyo.

Kama utataja majina ya watu waliowahi kutamba visiwani humu katika mchezo wa mpira wa meza na soka bila ya kumtaja Abdulwakati itakuwa hukumaliza idadi yao.

Abdullah Juma Aley ndio jina lake alilopewa na wazazi wake,lakini hata hivyo jina hilo linafahamika kwa watu waliokuwa sio wengi kwani ukipita katika mitaa mingi ya visiwani humu ikiwemo Kikwajuni na kumtaja jina la Abdullah hutompata mpaka utaje Abdulwakati.

Jina hilo ndio limekuwa maaarufu kuliko jina lake halisi kwa kipindi chote alichocheza michezo hiyo Zanzibar,Tanzania,Afrika Mashariki na hata Arabuni .
Mwandishi wa makala haya alimtafuta mwanamichezo huyo huko nyumbani kwake Michenzani na kuzungumza nae kwa kina katika mambo mbali mbali yanayomuhusu yeye kimichezo.

Alisema kwamba umaarufu wa jina la Abdulwakati hautokani na kitu chochote isipokuwa ni mchezo wa soka ambao ulimpatia umaarufu mwaka 1980 na kuendelea.
Alisema kwamba jina la Abdulwakati alilipata wakati alipokuwa mdogo akichezea timu ya hero Boys ambapo alisema jina hilo alibatizwa na mwalimu wake wa soka Abubakar Soni.

“Katika timu yetu kulikujwa na wachezaji watatu na wote walikiuwa na majina ya Abdul ,hivyo kutotufautisha sisi akaamua mimi kuniita Abdulwakati  kwa vile nilikuwa nachezea nafasi ya mshambuliaji wa kati,”alisema.

Mchezaji huyo mkongwe ambae kwa kawaida ni mcheshi,alisema wachezaji wenzake walibatizwa majina mengine kama vile Abdul Kikono na Abdul Kifupi.

Katika maisha yake ya soka,alianza kung’ara mapema utotoni mpaka kupewa mikoba ya unahodha kwenye timu ya shule visiwani Zanzibar.

Aliendelea kucheza timu ya watoto kabla ya kujiunga na klabu ya Everton iliyokuwa na maskani yake katika mtaa wa Kikwajuni mjini Unguja  mnamo mwaka 1970.

Kutokana na uwezo wake mkubwa wa kusakata kabumbu Abdulwakati alichukuliwa na timu iliyokuwa ikimilikiwa na kituo cha kulelea watoto cha Forodhan iliokuwa ikijulikana kwa jina la Karume Boys na kutembea nayo katika mikoa mbali mbali ya Tanzania.

Timu hiyo ambayo ilikuwa chini ya uangalizi wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar marehem Mzee Abeid Aman Karume ambapo timu hiyo ilikuja kugawanyika mara baada ya kifo cha kiongozi huyo mwaka 1972.

Akiwa katika kikosi hicho cha Karume Boys alikutana na wachezaji wengi akiwemo Sihaba Saadat,Omar Willium na wengine wengi.

Mnamo mwaka 1972 baada ya kusambaratika kwa Karume Boys,Abdulwakati alijiunga na kikosi cha Small Simba baada ya kushawishiwa kufanya hivyo na kocha wa zamani wa kikosi hicho ,Masoud Salim almaarud Maoud Kocha.


Kutokana na ari,jitihada na moyo wake wa kusakata kabumbu wakati anapokuwa uwanjani,veteran huyo alichaguliwa kujiunga na timu ya Taifa ya vijana ya Zanzibar mwaka huo huo 1972.

Akiwa na Small Simba,Abdulwakati alikuwa kivutio kikubwa sawa na wachezaji wote wa timu hiyo iliyojipatia umaarufu mkubwa baada ya kupanda daraja,ambapo ilianza kwa moto mkubwa na kutikisa vigogo vya soka nchini.

Alisema timu yao ilikuwa imesheheni vipaji na kuwa gumzo la mji na kuanza kujitwalia ubingwa wa soka visiwani mwaka mwaka huo huo waliopanda ngazi 1983.
Chini ya nyota mahiri akiwemo wakati,Small Simba iliweza kutamba vilivyo katika miaka 1985 hadi 1987.

“Kuanzia mwaka 1983 hapo moto wetu ulikuwa hauzimiki na mashabiki wetu wakapata wimbo wa ‘Moto Small’ambapo kila tulipokuwa tunashuka dimbani au watu walipokuwa wakizungumzia timu yetu waliimba Moto Small,alisema mwanandinga huyo.

Jambo ambalo nyota huyo atabaki akilikumbuka maishani kwake ni tukio la mwaka 1987 kwa timu ya Small Simba kupokonywa ubingwa na Miembeni ambao walikwenda mahakamani.

Anasema anafahamu kwanini walishindwa kesi hiyo na kila mmoja alijua kutokana na hakimu wa kesi hiyo alikuwa Miembeni damu,hivyo alisema haki haikutendeka.

Abdulwakati alisema kwamba sababu za kwenda mahakamani wenzao na kupokonywa ubingwa kumetokana na wenzao wa Miembeni kudai kwamba walimchezesha mchezaji Shaban Mussa ambae hakuwa halali,licha ya chama cha soka Tanzania (FAT) kuthibitisha mahakamani kuwa mchezaji huru.

Umahiri wake katika soka uliwashawishi wahusika wa juu kumuita kwenye timu kubwa mwaka 1984 na kushiriki katika michuano ya Chalenji iliofanyika mjini Mombasa nchini Kenya.

Milango ya kheri ikamfungukia siku chache baada ya kurudi kutoka Mombasa,ambapo mashushu wa Oman walikuwepo kusaka wachezaji wa kuwapeleka kwao.

Mwaka 1984 Abdulwakati alitua rasmin nchini Oman na kuanza kuwasuuza roho Waarabu  kwa ufundi wake wa kumiliki mpira na kupachika mabao.

Alisema mechi yake ya kwanza ilikuwa kati ya Oman na Qatar katika michuano ya ubingwa wa nchi za Ghuba akicheza kwa dakika 20 tu.

Aidha katika mechi ya kihistoria iliyochezwa Riyadh Saudi Arabia ikiwa ni michuano ya Gulf ushindi wa kwanza kwa Oman ulipatikana baada ya kurudi kambi nchini Brasil ambapo Abdulwakati alifanikiwa kuipatia timu yake goli moja na timu yake kuibuka na ushindi wa magoli 2-1.

Kutokana na kipigo hicho Qatar ilimkatika rufaa Abdulwakati kwa madai kwamba ni mgeni,lakini rufaa hiyo ilishindwa kwani nao pia walikuwa na wachezaji kutoka Somalia wawili.

Hata hivyo mchezaji huyo alikuwa halali kuchezea timu hiyo ya Oman kutokana na kufanyiwa taratibu zote za uraia.

Baada ya hapo akawa anapangwa mechi zote kwa dakika 90 na kuwashangaza matajiri wake kwa kipaji alichokuwa nacho.

Anakumbuka matokeo mazuri ni yale ya sare1-1 walipocheza na U.A.E ambao ni wapinzani wakubwa wa Oman sawa na timu za Kenya na Uganda.

Anafahamisha kwamba kila mwaka Oman ilikuwa ikishika mkia katika mashindano ya ‘Gulf Cup’ lakini katika mashindano hayo walishika nafasi ya nne kati ya nchi sita.

Pamoja na mafanikio makubwa aliyoyapata katika nchi ya Oman,mchezaji huyo anakumbuka kadhia iliyowakasirisha wachezaji baada ya kutwaa ubingwa wa Ghuba ambapo chama cha soka na Wizara husika kushindwa kutimiza ahadi zao kwamba wangewapa zawadi nono.

Akiwa na timu hiyo,mwanasoka huyo veteran alifanikiwa kwenda katika nchi zote za ghuba kushiriki michuano yao inayochezwa kwa zamu.

Katika kumbukumbu yake alifahamisha kuwa wakati wakijiandaa na mashindano ya Bahrainwalipiga kambi nchini Ufaransa na akabahatika kufundishwa na kocha Omar Boras raia wa Uruguay mwaka 1988 hadi 1990, ambae alikuwa kocha wa nchi yake katika mashindano ya kombe la dunia yaliofanyika Mexico mwaka 1986.

Baada ya kumaliza waliyotumwa kwa Oman kuwa mabingwa wa Ghuba zilizjitokeza baadhi ya timu kumtaka na hatimae alijiunga na klabu maarufu ya Fanja ilioko nchini Oman.

Wakati huo alisema alikuwa ni Mtanzania wa kwanza kujiunga na Fanja mwaka 1985,kabla ya kina Ahmed Amasha,Talib Hilal,Zahor Salim na Hilal Hemed.
Akiwa na timu hiyo aliiwezesha kutwaa ubingwa wa Oman mara nyingi sambamba na kombe la Sultan Qaboos kuanzia mwaka 1985 hadi 1992.

Aidha alisema mwaka 1987 alirudi Zanzibar kwa ajili ya mapumziko na kwenda na timu ya taifa nchini Ethiopia kwenye Chalenji ambapo walitoka sare na Kenya huku Tanzania Bara wakiifunga magoli 2-0  na kutoka sare na Ethiopia katika mechi ambayo mlinda mlango alikuwa Ali Bushiri ambae aliokoa kwa penalti.

Hata hivyo kikosi hicho kilichokuwa kikinolewa na makocha Gulam Abdallah na marehemu Mzee Kheri kilitolewa na Zimbabwe katika hatua ya nusu fainali.

Anaelezea kitendo cha muamuzi kuwabeba Wazimbabwe kilichangia kufungwa kwani walipokua nyuma kwa mabao 2-1, Inocent Haule alisawazisha lakini likakataliwa.

Abdulwakati ambae tangu akiwa kinda,alikuwa na lengo la kuchezea soka la kulipwa,anasema aliwahi kushawishiwa na viongozi wa Simba wakati huo akiwa na timu ya Taifa Stars lakini aligoma kwa vile hakuyaka kuihama Small Simba.

Kwa upande wa mechi ambayo anaikumbuka akiwa na klabu ya Small Simba,siku moja walikwaaana na Yanga katika Michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) ambayo ilifanyika Mombasa Kenya.

Anasema Small Simba wakiwa nyuma kwa magoli 2-0  hadi mapumziko, ndani ya chumba cha kubadilisha nguo alimuomba kocha Abdulghani Msoma amtoe nahodha Fadhil Ramadhani.

Anasema kufuatia mabadiliko hayo wakaweza kurudisha bao moja na ikiwa zimebakia dakika 10,mchezaji mwezake aliemtambulisha kwa jina la Kirara ambae kwa sasa ni marehemu  alimzidi maarifa Juma Mkambi kasha akatulia na mpira akaja akamtoboa tena na kutoa pasi kwa Rashid Khamis aliepachika bao la pili.

Kwa upande wa mabeki ambao walikuwa wakimpa tabu wakati huo na timu zao kwenye mabano ni Hassan Wembe(Malindi), Abdallah Rajab(KMKM) na Said Ibrahim Njunju(Miembeni).\

Mwanandinga huyo alisema kwamba alikuwa akijisikia fahari sana akiona anacheza na kikosi kizima cha Small Simba lakini zaidi akiwa na Yussu Kassim na marehemu Kassim Kirara na mabeki Khamis Suleiman ‘Mpemba’ na Khalfan Ukasha.

Aidha Abdulwakati hakuacha kusifia umahiri wa mlinda mlango wa zamani wa wapinzani wao Black Fighters,Mwinjuma Makungu (marehemu) kwa ujasiri wake wa kuzuia michomo akiruka kwa staili ya kipekee.

Anasema kwamba kwa kiasi kikubwa soka limemsaidia kufika katika nchi mbali mbali kama Algeria, Misri,Zambia,Ufaransa,Brazil na nchi zote za falme za kiarabu Malaysia na Thailand.

Lakini mbali na kuwika katika mpira wa miguu,Abdulwakati alikuwa mahiri katika mchezo wa mpira wa meza (Table teniss) ambapo lifanikiwa kuchezea katika ya Taifa ya Tanzania na timu ya Taifa ya Zanzibar na kuwa mchezaji nambari moja nchi nzima.

Abdulwakati alihamisha kwamba mwaka 1974 aliiwakilisha Tanzania huko Alexandra Misri na kutolewa katika hatua za awali,ambapo mwaka 1977 alishiriki katika mashindano ya Tanzania Table Teniss kwa nafasi ya senior na bahati nzuri alichukua ubingwa wa mchezo huo kwa Tanzania nzima.

Abdulwakati aliweza kufanikiwa kuchukua ubingwa wa Tanzania kwa miaka minne mfululizo katika michuano ya Coastal Town Champion Ship ambayo ilikuwa ikichezwa katika jiji la Dar es Salaam,Tanga na Mombasa katika kipindi cha Sikukuu za Pasaka.

Mwaka 1978 mwanamichezo huyo sambamba na wenzake walibeba bendera ya Tanzania kwenye michuano ya Afrika (All African Games) nchini Algeria.

Katika mashindano hayo alitolewa na Nigeria katika robo fainali na kusema kwa kawaida  Wamisri na Wanigeria katika mchezo wa mpira wa meza.

Mwaka huo huo wa 1978,Abdulwakati aliungana na wenzake kutoka katika Mikoa ya Tanzania kushiriki katika mafunzo ya miezi sita kwa mchezo huo na kufundishwa na aliekuwa bingwa wa dunia,Liyanko Liyang.

Aliwataja wachezaji wenzake aliokuwa nao ni pamoja na Fatma Jidawi,Narman Jidawi,Shaaban Umiki,na Mohammed Salum wote kutoka Zanzibar ambapo kutoka Tanzania Bara ni Ahmed Diwani na Lucas Kiwango.

Alifafanua kwamba kikosi cha mpira wa meza Zanzibar kilikuwa kizuri kutokana na mafunzo waliyokuwa wakiyapata kutoka kwa kocha wao Wu Li Yen ambae alikuwa Balozi mdogo wa Jamuhuri ya Watu wa China.

Hivi sasa Abdulwakati amekuwa akijumuika na wachezaji Veterani wengine hapa nchini kuunda timu ya Wazee Sports Club inayofanya mazoezi yake kwenye viwanja vya kila siku jioni.

Kuhusu utofauti wa soka la zamani na sasa,Abdulwakati alisema soka la zamani lilikua na tofauti kwani wachezaji wake walikuwa hawapati nafasi ya kucheza soka la kulipwa katika nchi za Ulaya tofauti na sasa.

Aliongeza kwamba wachezaji wa zamani walikuwa wakicheza kwa ari na nguvu zote tofauti na ilivyo kwa wachezaji wa sasa kwani wamekuwa wanacheza kwa tamaa na fedha zaidi na sio moyo wa kuzipenda timu zao.

Mchezaji huyo mkongwe aliwashauri wachezaji hao kutopendelea kutumia vitu hivyo ambavyo havitoweza kuwajengea viwango vyao katika uchezaji wa soka.

Huyo ndie Abdulwakati aliezaliwa mwaka 1959 katika mtaa wa Kikwajuni mjini Unguja na kuanza elimu ya msingi katika shule ya Darajani mwaka 1967 na baadae kumalizia masomo yake katika shule ya Vuga mwaka 1976.

Baadae wazazi wake walimpeleka Mkoani Morogoro kwa ajili ya kurejea masomo yake ya kidato cha tatu na cha nne katika Shule ya kilimo ya Ifakara.

Abdulwakati ni baba mwenye familia ya watoto wawili Nawwal na Nageeb,hivi sasa ni muajiriwa katika kampuni ya usafiri wa Anga Zanzibar (ZAT).





Wednesday, 10 June 2015

TAUSI WOMEN TAARAB: KUNDI LINALOPIGA MUZIKI WA TAARAB KWA KUTUMIA ALA ZA ASILI


TAUSI ni mmoja wa ndege maarufu ambae ni mrembo alieumbika kutokana na umbo lake zuri la kupendeza,uzuri huo pia huonekana kwa manyoya yake ambayo pia ni kivutio kwa wengi wakiwemo watoto wadogo.


Nyimbo mbali mbali ziliwahi kuimbwa ambazo zinaonyesha kumsifia ndege huyo na kuonekana kuvuta mapenzi kwa watu wengi,lakini pia uzuzri wa ndege huyo kumefanya hata kupatikana kwa jina la la mtu kwa uzuri wake.

Lengo langu sio kumsifia wala kumzungumzia ndege huyo ,bali ni kuzuzngumzia mustakabali mzima wa kundi la taarab la akina mama ambalo limeweza kujizolea umaarufu mkubwa sana ndani nan je ya visiwa vya Zanzibar.

Mara baada ya kuona kazi zinazofanywa na akina mama hao mwanzo mwa mwezi huu katika tamasha la Sauti za Busara hamu na shauku kubwa ilinipata ya kutaka kujua kiundani azma na lengo la kuanzishwa kwa kundi hilo.


Niliweza kufika katika Makao Makuu ya Klabu hiyo yalipo katika maeneo ya Kisiwandui mkabala na Msikiti Mabati mjini Unguja na kukutana na Mkurugenzi wa kundi hilo Bi Maryam Hamdani.

Bi Maryam alinielezea tangu kuanzishwa kwake,walipofikia na matumaini ya baadae ya kundi hilo .

Tausi ni kikundi pekee nchini Tanzania kinachopiga muziki wa taarab asilia ambacho kinafanya shughuli zake zote kupitia akina mama wanaoongozwa na Mkurugenzi huyo anaepiga ala ya Qanoon.

Sio jambo la rahisi kuona akina mama hao wanaweza kufanya kazi hasa ya kupiga ala asilia ambazo ni ngumu kutokana na ala hizo kutumika bila ya umeme na ndio jambo lililonifanya niamini kwamba wanawake wakiamua wanaweza.

Jina la Tausi limetokana na Mkurugenzi huyo kumpenda ndege huyo tangu akiwa mdogo na alisema kuwa mapenzi yake yalikuwa kwa ndege wawili ambae ni Tausi na Ziwarde na ndipo akaamua kukiitia kikundi hicho kwa jina la Tausi.

“Tangu utoto wangu Tausi na Ziwarde nilikuwa nawapenda sana nikaamua nikaamua kukiita kikundi hichi jina la ndege huyu na pia nilitaka kubadilisha majina ya vikundi vya taarab na sio kila siku hayo kwa hayo,”alisema Bi Maryam.


Tausi ilizaliwa rasmin Julai mwaka 2009 kikiwa na vijana wa kike 22 ambapo alianza nao kwa kuwafundisha kupiga ala mbali mbali akiwa yeye na walimu wenzake Marehemu Iddi Abdallah Farahan,Mohammed Ilyas,Ramadhan Muhidin na Ali Ibrahim.

Walianza kwa kuwafundisha kutumia ala mbali mbali ikiwemo Qanoon,Udi,Fidla,Violin,Tablah,Key board, Bongos na aina mbali mbali za ala ambazo zinatumika katika muziki wa taarab asilia.

“Hamu yangu ya kupenda muziki wa taarab na mimi mwenyewe nikiwa msanii na pia nafahamu kutumia ala ya Qanoon ndio niaamua kuanzisha kikundi hichi ambapo nilianza na akina mama 22,”alisema.

Mara baada ya kuonekana kwamba upo umuhimu kutokana na kuanzishwa kwa kikundi hicho watu mbali mbali wenye hamu ya kuwa wasanii ambao wanahitaji kujifundisha kutumia ala walianza kujiunga na Tausi.

Mkurugenzi huyo anafahamisha kwamba sharia ya kikundi hicho kuwa hakuna msanii yoyote aliekuwemo ndani ya Tausi lazima ajue kupiga ala na sio kubakia kwenye kuimba tu.

“Wapo wasanii ambao walijiunga na Tausi wakiwa hawajuai chochote zaidi ya kuimba tu,lakini nashukuru kutokana na jitihada ya Tausi na sharia yetu watu wote wajue kupiga ala basi sasa hivi takriban wasanii wetu wote wanajua kutumia ala,”alifahamisha.

Hakuna jambo lizilokuwa na matatizo wala faida,lakini kwa upande wa matatizo yanayokikabili kikundi hicho ni ukosefu wa vifaa ikiwemo kukatika kwa  nyuzi ambazo zinatumika kwenye ala na matatizo mengine amabayo alisemani ya kawaida tu.

Lakini kwa upande wa faida,Tausi imeweza kupata faida mbali mbali ikiwemo kujua kupiga ala,kujiajiri wenyewe kujua zaidi kutumia ala za asili,kupiga taarab katika sehemu mbali mbali na kuweza kusafiri.

Mkurugenzi huyo alizitaja sehemu ambazo wamebahatika kufanya maonyesho ni katika matamasha ya busara kwa miaka mitatu,sherehe za mkutano wa EU sherehe za chakula cha usiku kwa wadau wa elimu pamoja na uzinduzi wa mkutano mkuu wa AU uliofanyika mjini Nairobi na kuhudhuriwa na alikekuwa Makamo wa Rais wan chi hiyo Raila Odinga.

Lakini pia Mkurugenzi huyo alisema kujwa faida nyengine kwa kundi hilo ni kuhudhuria katika matamasha ya kimataifa yaliofanyika nchini Lebanoon na Misri.

“Hii ni faida kwetu na faraja iliyoje kupata kufanya maonyesho katika sehemu mbali mbali tena kubwa ambazi imeweza kutusaidia kukitangaza kikundi chetu pamoja na nchi yetu kwa ujumla,”alieleza.

Aidha kundi hilo pia limeweza kupiga nyimbo mbali mbali pamoja na Bashraf zao wenyewe ambazo zimetungwa katika kundi hilo ambapo miongoni mwa watunzi hao akiwa yeye mwenyewe Mariam Hamdani.

Tausi linatamba na nyimbo zake mbali mbali zikiwemo Usione vyaelea,Walodhani mzaha,Nibembeleze,Si rahisi na dhana ambapo kwa upande wa bashraf zinajuliakana kwa jina la Tausi na Alya.

“Kundi letu limeweza kutunga nyimbo pamoja na bashraf  ambapo tunapokwenda katika maonyesho huwa tunapiga nyimbo zetu wenyewe,”aliongezea Mkurugenzi huyo.

Aidha kwa upande wa matarajio ya kikundi hicho Maryam alisema ni matarajio yao kuwasomesha wasanii wa kundi hilo ndani nan je ya Zanzibar ili waweze kuwa wasanii watakaoitangaza vyema Zanzibar.

“Matarajio yetu Tausi ni kuwapa mafunzo yalio bora wasanii wetu ambayo watayapata ndani nan je ya Zanzibar ili wawe wasanii bora ambao wataitangaza Zanzibar kupitia fani hii ya muziki wa Taarab asilia,”alisema.

Mbali na hayo lakini pia malengo mengine ya Tausi ni kupata wasanii bora wa kike ambao ambao wataweza kutunga mashairi ambayo yatasaidia kuwainua wanawake na pia kutafuta klabu maalum .

Alifahamisha kwamba lengo la kutafuta klabu ni kutaka kuendelea kwa kikundi hicho ambapo alifahamisha kwamba vikundi vingi  sana vya taarab vinakufa kutokana na kukosekana kwa klabu .

Maryam Hamdani ambae pia ni Makamo wa Rais wa Baraza la Habari Tanzania (MCT)  amewashauri wasanii kuendeleza muziki wa taarab asilia ili waweze kuitangaza nchi yao kupitia fani hiyo.

Pia aliwashauri wanawake kutumia fani hiyo kuwa ni ajira na sio kuifanya fani hiyo kuonekana kuwa ni fani ya kihuni jambo ambalo alisema kuwa sio kweli bali ni dhana potofu kwa watu wasiopenda fani hiyo.

Kutokana na sababu mafanikio hayo,Mkurugenzi wa Tausi ambae pia ni mwanzilishi wa kundi hilo ana kila sifa ya kupewa kutokana na ujasiri wake alionao katika kusaidia kutetea haki za wanawake wenzake katika Nyanja ya muziki wa taarab.

Hii ni faraja kubwa kwa nchi yetu kutokana na mama huyo kuona umuhimu kundi hilo na hakuna budi kwa taasisi mbali mbali za Serikali na binafsi kukisaidia kikundi hicho ili kiweze kukuwa na kuwapatia ajira akina mama hao.

Tausi ambalo ni kundi maarufu likiwa chini ya mlezi wake aliekuwa Waziri wa Fedha za zamani wa Jamuhuri ya Muungano wam Tanzania Zakia Meghji linaendelea kufanya maonyesho yake katika sehemu mbali mbali za mjini na mashamba.